Wednesday, February 13, 2013

WADAU WA ELIMU KIBAHA

Ben Komba/Pwani-Tanzania/12 February, 2013/14:40:45

Masuala ya ruzuku na kukosekana kwa walimu wa kike wa kutosha katika maeneo ya pembezoni kumezua mjadala wa kadiri katika kikao cha wadau wa elimu katika halmashauri ya wilaya Kibaha, chenye lengo la kung'amua mafanikio na mapungufu katika suala zima la usimamizi wa elimu.

Mmoja wa wajumbe waliohudhuria kikao hicho kutoka katika Kata ya Magindu amelalamikia idara ya elimu kwa kuzorotesha upelekaji wa ruzuku ya dola kumi kwa kila mwanafunzi na hivyo kuathiri uboreshaji wa elimu, amefafanua upatikanji wa fedha hizo umekuwa na mizengwe mingi na hata zikipatkana zinakuwa zimeshachelewa.

Mjumbe huyo ameitaka serikali kuhakikisha inafikisha fedha za ruzuku kwa wakati na wachukulie suala hilo kama wajibu na sio hisani kama watendaji wengi wanavyolichukulia na kusaidia kuwaepusha baadhi ya watendaji kujikuta wanatoa fedha za mifukoni mwao kuendesha shughuli za shule.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya shule ya msingi MUYUMBO, BW. MORETO MORETO amebainisha tatizo la walimu wa kike katika shule yao, jambo ambalo linawapa wakati mgumu wanafunzi wa kike wanapopatwa na matatizo yanayosabishwa na maumbile yao.

Hivyo ameitaka idara ya elimu kuwa na utamaduni wa kutembelea shule hiyo mara kwa mara kwani kuna uchakavu mkubwa wa majengo na samani za shule, tatizo ambalo linachangiwa na kutokuwepo kwa wakaguzi wa kupitia shule na kuziangalia maendeleo yake kama ilivyokuwa zamani.

Afisa elimu msingi halmashauri ya wilaya ya Kibaha BIBI. WINFRIDA MBUYA akijibu hoja za wajumbe hao wawili amesema suala la ruzuku kwa shule za msingi hilo ni tatizo la Hazina ambapo yeye kwa nafasi yake hawezi kulisemea kutokana na taarifa ya kutokuwepo kwa fedha za kutosha kukidhi mahitaji yanayohusiana na idara yake, na kuhusiana na suala la shule ya msingi ya Muyombo yeye kasema huwa wanaitembelea.

No comments:

Post a Comment