Bw Joseph Kabila ametangazwa mshindi wa urais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Kulingana na tume ya uchaguzi ya nchi hiyo Joseph Kabila ameshinda kwa
asilimia 48, mpinzani wake mkuu Etienee Thisekedi akiwa na asilimia
32.33 na Vital Khemere naye akipata asilimia 7.74.
Wapinzani wamelalamika kuhusu kuwepo udanganyifu na usalama
umeimarishwa kwenye mji mkuu, Kinshasa, huku kukiwa na wasiwasi wa
kutokea ghasia.
Polisi wa kuzuia ghasia wanafanya doria kwenye mitaa ya mji mkuu huo, unaoonekana kuwa ngome ya upinzani.
Maduka mengi yalifungwa kwenye soko la Kinshasa kwa takriban wiki nzima.
Mkuu wa tume wa uchaguzi Daniel Ngoy Mulunda, "
Tume huru ya uchaguzi wa taifa inathibitisha kuwa Kabila Kabange Joseph
amepata kura nyingi zaidi".
Katika mji wa Goma mashariki mwa nchi hiyo, watu
walianza kushangilia matokeo tu yalipotangazwa katika televisheni na
redio ya taifa, ameripoti mwandishi wa BBC Joshua Mmali.
Matokeo hayo bado yanahitaji kuidhinishwa na mahakama kuu.
Bw Kabila amekuwa rais tangu mwaka 2001, kufuatia kifo cha baba yake Laurent.
Mwaka 2006 alishinda uchaguzi wa kwanza tangu
kumalizika kwa mgogoro wa miaka mitano na sasa anatarajiwa kuapishwa
Desemba 20 kwa muhula wake wa pili.
No comments:
Post a Comment