Monday, December 19, 2011

Barcelona mabingwa wa kandanda duniani

Barcelona wameshinda kombe la dunia la Fifa kwa vilabu baada ya kuicharaza timu ya Santos ya Brazil kwa mabao 4-0 kwenye mchezo wa fainali uliyochezwa nchini Japan.
Ushindi huo umeendeleza rekodi nzuri ya klabu hiyo kwa mwaka huu ambapo wao ni mabingwa wa Ligi ya Hispania maarufu La Liga, wanashikilia ubingwa wa vilabu vya Ulaya na pia Kombe la Hispania maarufu Spanish Super Cup.
Mpachika mabao wa timu ya taifa ya Argentina Lionel Messi alifunga mabao mawili, huku mengine yakiwekwa kimiani na Xavi pamoja na nahodha na kiungo wa zamani wa Arsenal Cesc Fabregas.
Ushindi huo unathibitisha kwamba Barcelona inaendelea kusalia timu bora ya kusakata kandanda duniani.
"Tulicheza mchezo wetu kwa ukamilifu," alisema nahodha Carles Puyol. "Ulikuwa mchezo mzuri, mchezo mgumu sana na tumefurahi sana kwa matokeo haya."
Mchezo huo baina ya mabingwa wa kandanda wa Ulaya na wa Amerika Kusini mjini Yokohama ulikuwa ukitajwa kuwa kivutio kati ya Messi, anayeaminika ndiye mchezaji bora wa soka duniani na mshambuliaji hatari wa Brazil mwenye umri wa miaka 19 Neymar, ambaye anatajwatajwa huenda akajiunga na ama na Barca au Real Madrid.
Lakini haikuwa hivyo - Messi akionekana kushamiri katika mchezo huo na kutajwa mchezaji bora wa mechi hiyo na pia akapata tuzo ya mchezaji mwenye thamani kubwa katika michuano hiyo wakati Barcelena ikiweka kibindoni kombe la ubingwa wa dunia kwa mara ya pili mfululizo katika misimu mitatu.
Bao lake la kwanza alifunga kwa kuubetua mpira kama ilivyo kawaida yake na la pili alifunga kwa ustadi mkubwa baada ya kumzunguka mlinda mlango wa Santos Cabral.
Santos walibadilika na kucheza soka nzuri kipindi cha pili na Neymar nusura afunge baada ya kupatiwa pasi nzuri akiwa amebakia peke yake na mlinda mlando wa Barcelona Victor Valdes, lakini Valdes akafanikiwa kuokoa.
"Barcelona walistahili kushinda. Ni timu bora duniani na tumejifunza somo muhimu," alisema Neymar.
Timu ya Qatar ya Al Sadd, ambayo ililazwa mabao 4-0 na Barcelona katika hatua ya nusu fainali, iliwafunga mabingwa wa Japan Kashiwa Reysol mabao 5-3 kwa mikwaju ya penalti na kufanikiwa kushika nafasi ya tatu ya michuano hiyo inayofanyika kila mwaka kwa kushirikisha mabingwa wa soka wa mabara duniani.

No comments:

Post a Comment