Mbeya. Msaidizi wa zamani wa Padri (Katekisita) katika Kigango
cha Kanisa Katoliki Kijiji cha Mkwajuni, Florian Mwamosi (70) amekufa
baada ya kuzikwa akiwa hai katika kaburi moja na mtu anayedaiwa kumuua kwa njia
ya kishirikina.
Tukio hilo limetokea katika Kitongoji cha Maweni kijijini hapo
wilayani Chunya mkoani Mbeya.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Diwani Athumani alikiri
kutokea kwa tukio hilo akieleza kuwa lilitokea saa 9:00
mchana katika kijiji hicho cha Maweni Mkwajuni wilayani Chunya.
“Marehemu aliuawa na wananchi wenye hasira kali kwa kupigwa na
mawe kwa tuhuma za kuhusika na uchawi na kusababisha kifo cha Peter Robert,”
alisema.
Kamanda Athumani alisema kuwa uchunguzi kuhusiana na tukio hilo
unaendelea na kwamba wahusika wote wa tukio hilo wamekimbia na kuzihama nyumba
zao, hivyo polisi wanaendelea na msako wa kuwatia mbaroni watuhumiwa na kwamba
tayari kaburi hilo limefukuliwa jana kutenganisha maiti hizo.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa marehemu huyo ambaye
alikuwa akituhumiwa kwa ushirikina aliwahi kuwa Katekista wa kigango hicho hadi
mwaka 2007.
Wameeleza kuwa Mwamosi alikwenda kuhudhuria mazishi ya
Peter Robert (28) katika kitongoji hicho cha Maweni, baada ya
kufuatwa nyumbani kwake na watu wakitaka aende kwa sababu yeye ni mmoja wa
wazee wa mila katika kitongoji hicho.
“Bwana Mwamosi alikuwa akituhumiwa kwa uchawi kwa muda mrefu na
wenzie wawili, hivyo alipofika makaburini ilianza minong`ono ya watu na
huku wengine wakiguna na ndipo alipoombwa aingie kaburini kwa ajili ya
kupokea jeneza lililobeba mwili wa marehemu Peter Robert,” alisema mkazi
mmoja wa kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina moja la Joseph.
Alisema kuwa baada ya kuingia kaburini akiwa na watu wengine
watatu wenzake walitoka kwa haraka na kumwacha Mwamosi peke yake ndipo kundi la
watu waliokuwa eneo hilo la makaburi walianza kumshambulia kwa kumpiga mawe
huku wakimwamuru akae chini.
Shuhuda huyo alisema kuwa baada ya kukubali kukaa chini akiwa
ndani ya kaburi hilo, walianza kumfukia na alipofukiwa nusu ya mwili wake
waliingiza jeneza la marehemu Peter na kuliweka juu yake na kuanza kulifukia
kaburi hilo.
“Baada ya kukaa chini ndani ya kaburi hilo ndipo walianza kumfukia
kwa udongo na baadaye wakachukua jeneza la marehemu na kuliweka juu yake, kisha
kumfukia na udongo na taratibu za mazishi ziliendelea kwa ajili ya
marehemu Peter,”alisema.
Alidokeza kuwa chanzo cha tukio hilo ni marehemu Robert kuugua
ghafla tumbo, ndipo ndugu zake walipoamua kumpeleka kwa mganga wa jadi kwa
ajili ya kupata matibabu na baada ya siku tatu alifariki dunia.
No comments:
Post a Comment