Wednesday, September 19, 2012

USTAADH JUSSA ALIPOFUNGUKA UCHAGUZI WA BUBUBU



"Uchaguzi mdogo wa Bububu: Mengi yamesemwa toka jana. Naziona hamaki na hasira, nazihisi hisia za kukata tamaa na kutafishika. Uchaguzi wa Bububu ulikuwa ni zaidi ya uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi ya Mwakilishi. Haukuwa uchaguzi kati ya CUF na CCM kama wengi walivyodhania au walivyoutazama. Ulikuwa ni mfano wa kura ya maoni ndogo kuhusu mwelekeo wa nchi yetu. Ulikuwa ni uchaguzi kati ya wapenda maridhiano na wayachukiao. 

Ulikuwa ni uchaguzi kati ya wapenda maendeleo na wahafidhina. Lakini kubwa zaidi ulikuwa ni uchaguzi kati ya wanaotaka Jamhuri ya Watu wa Zanzibar yenye mamlaka kamili kitaifa na kimataifa na wale vibaraka wanaotaka Zanzibar iendelee kuwa koloni la Tanganyika. Umma ulipoonekana kuwa upande wa wanaopenda maridhiano, wanaotaka maendeleo na wanaoitaka Zanzibar yenye mamlaka kamili,
 watawala wakijumuika kati ya vibaraka waliopo Zanzibar na wakoloni wanaowatumikia wakaamua kutumia nguvu kubwa ili kujaribu sauti ya nguvu hiyo isitoke.

Wasichokijua ni sauti imetoka na imesikika, tena bila ya kisisi. Balozi Seif Ali Iddi (katika comment moja jamaa alimwita Balozi wa Tanganyika nchini Zanzibar) na wenziwe wanaotumikia agenda ya Tanganyika hapa Zanzibar walidhani kwa kutumia nguvu ile kubwa watatuyumbisha na kutuhamakisha tuivunje Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambayo yeye na wenzake hawakuahi kuiamini wala kuiunga mkono na kwa kufanya hivyo wakadhani watafanikiwa kuyavunja maridhiano na umoja wa Wazanzibari.

 Wakadhani wakifanikiwa katika hilo watakuwa wamevunja umoja na ari ya Wazanzibari kudai nchi yao. Wamepwerewa wao na mabwana wanaowatumikia. Akili zetu razina. Haondoki mtu kwenye mstari. Tutayalinda maridhiano na umoja wa Wazanzibari. Na tutalilinda na kulipeleka mbele vuguvugu la Wazanzibari linalojumuisha makundi na taasisi tofauti kuirudisha Zanzibar yetu".
<

No comments:

Post a Comment