Thursday, June 7, 2012

MATUMIZI YA NDEGE ZISIZO NA RUBANI YALETA KIZAAZAA

Ndege zisizo na rubani


Waziri wa Ulinzi wa Marekani Leon Panetta ameteta hatua ya Marekani kutumia ndege zisizo na rubani kushambulia wanamgambo nchini Pakistan,siku mbili baada ya shambulizi la makombara kumuua kiongozi wa kundi la al-Qaeda, Abu Yahya al-Libi.
Panetta alisema kuwa Marekani ilielezea msimamo wake bayana kuwa itaendelea kutumia ndege hizo kujilinda.
Alitoa matamshi yake wakati akihudhuria mkutano katika nchi jirani ya India. Hapo jana Pakistan ilimtaka balozi wa Marekani nchini humo kuelezea tena wasiwasi wa Pakistan kuhusiana na matumizi ya ndege hizo dhidi yake.
Ndege nane kama hizo zimeshambulia maeneo ya wanamgambo nchini Pakistan katika wiki mbili zilizopita licha ya serikali ya Pakistan kutaka Marekani kukomesha mashambulizi hayo.
Kwa upande wake Pakistan inasema kuwa mashambulizi kutumia ndege hizo, yanachochea hisia zaidi za chuki dhidi ya Marekani na inadai kuwa raia wasio na hatia wamejeruhiwa katika mashambulizi hayo.
Hata hivyo Marekani inasisitiza kuwa mashambulizi hayo yamekuwa na faida kubwa katika vita vyake dhidi ya Al Qaeda hususan katika eneo lenye wanamgambo la mpakani mwa Pakistan na Afghanistan.
Maafisa wa Marekani wanasema kuwa kiongozi wa Al Qaeeda Abu Yahya al-Libi, alifariki katika shambulizi la makombora mawili katika mojawapo ya makaazi ya wanamgambo mashariki mwa mji wa Miranshah

No comments:

Post a Comment