Monday, December 12, 2011

MLINZI AWAPORA MAJAMBAZI SILAHA

Salum Maige, Sengerema
MLINZI wa Kampuni ya Mass Security Gambeta  amefanikiwa kupambana na watu saba wanaodhaniwa kuwa majambazi na kumwua mmoja kisha kuwapora bastola.

Mauaji hayo yalitokea baada ya zaidi ya dakika 30 za kurushiana risasi baina ya mlinzi huyo na majambazi hayo, yaliyotokea katika maduka ya kijiji cha Mbugani kilichoko kwenye Kata ya Bulyaheke wilayani Sengerema, Mwanza.

Katika mapambano hayo mlinzi huyo alifanikiwa kumpiga risasi ya mguuni mmoja wa majambazi hao na kuanguka na kumchapa mwingine risasi iliyomfanya aangushe bastola na kukimbia.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mbungani, Msiba Etangi alisema tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia juzi Jumamosi majira ya saa nane usiku, wakati majambazi hayo yakijiandaa kuiba katika maduka ya wananchi wa kijiji hicho yanayolindwa na kampuni hiyo.

Jambazi lililouawa limetambulika kwa jina moja la Juma linakadiriwa kuwa na umri usiozidi miaka 28 na kwamba makazi yake yako jijini Dar es Salaam lakini awali linadaiwa lilikuwa likiishi wilayani Geita mkoani Mwanza.

Mwenyekiti alifafanua kuwa jambazi hilo baada ya kupigwa risasi na kuanguka chini lilikutwa na bunduki moja aina ya SMG na kwamba kabla ya kukata roho liliwataja baadhi ya watu waliokuwa wakishirikiana nalo katika tukio hilo baadhi yao wakiwa wakazi wa kijiji hicho na wengine wa kijiji jirani cha Kanyala.

''Majambazi hayo yalikuwa na bunduki, mapanga, marungu na jiwe kubwa fatuma na yalikuwa yakijiandaa kupora kwenye moja ya maduka ya hapa, lakini mlinzi alipobaini kuwa ni wahalifu alipambana nayo kwa muda wa dakika 30 na akawa amelipiga limoja risasi miguuni na kuanguka. Baada ya kulipekuwa tumekuta likiwa na bunduki moja SMG ambayo nafikiri lilikuwa likitumia wakati wa mapambano na mlinzi huyo,'' alisema.

Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Liberatus Barrow alipotafutwa kwa  njia ya simu kuzungumzia tukio hilo alisema hana taarifa na kuahidi kuongea na wasaidizi wake ili apate taarifa zaidi kama kuna tukio kama hilo''.

Kwa upande wake kamanda wa Polisi Wilaya ya Sengerema, OCD Pundensiana alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo alisema yeye sio mzungumzaji licha ya kukiri kuwepo kwa tukio hilo na kwamba alituma askari wake eneo la tukio kufuatilia.

''Ndugu yangu mimi sio msemaji lakini tukio hilo lipo, nafikiri hebu mpigie aliyekupa hizo taarifa akupe maelezo jinsi tukio lilivyotokea, lakini nimetuma askari kufuatilia na kufanya uchunguzi kwa hiyo na wewe fuatilia,'' alisema.
 
Hata hivyo mwenyekiti wa kijiji hicho, Etangi alisema watu wanne waliotajwa na jambazi hilo kabla ya kukata roho walikamatwa na polisi waliokuwa wamefuatilia tukio hilo  kwa amri ya kamanda wa polisi Sengerema.

No comments:

Post a Comment