Thursday, May 17, 2012

waalimu huko PWANI

  • Ben Komba/Pwani-Tanzania/17-May-12/05:29:34 PM

    Zaidi ya shilingi milioni 455 zitatumika katika ujenzi wa jengo la chama cha walimu mkoa wa Pwani, ikiwa ni moja ya majengo yanayokusudiwa kujengwa kila mkoa katika kuhakikisha chama hicho kinajiimarisha kiuchumi kwa kujenga vitega uchumi ambavyo vitaongeza kipato na usalama wa maisha ya Mwalimu mara baada ya kustaafu utumishi.

    Katibu wa Chama cha Walimu Mkoa wa Pwani, MWL. NEHEMIAH JOSEPH amemweleza mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha kuwa chama chao kinategemea kukamilika kwa ujenzi wa jengo lao la ghorofa mbili ambalo linajengwa na kampuni ya SUMA JKT katika mwezi Septemba, ambapo litakapokamilika jengo hilo litakuwa na ofisi za chama cha walimu mkoa na wilaya, Benki ya walimu, ukumbi wa mikutano na ofisi nyingine zitapangishwa kwa wahitaji.

    MWL. JOSEPH ameongeza mradi huo wa kujenga ofisi utaendelea mpaka ngazi ya wilaya ambapo mpaka sasa katika mkoa wa Pwani wilaya ambazo zina ofisi zao wenyewe ni wilaya ya Rufiji ofisi yake imeshakamilika, wilaya ya Bagamoyo na Kisarawe ofisi zao zipo katika hatua za mwisho kuelekea katika kukamilika.

    MWL. NEHEMIAH JOSEPH amefafanua mpaka sasa wilaya ambazo hazina ofisi lakini zipo katika mchakato wa kujenga ofisi zao ni Mkuranga, Mafia na Kibaha ambao bado wanatafuta kiwanja, ujenzi huo ni mafanikio ya Jengo la Mwalimu HOUSE ambapo kupitia kitegauchumi hicho chama chao kimekuwa na kiu ya kufanya vizuri kutokana na mapato yanayopatikana na MWALIMU HOUSE kutumika kujenga ofisi katika kila mkoa.

    Aidha ameongeza sehemu kubwa ya fedha za ujenzi wa ofisi za Chama cha walimu katika kila mkoa ni nguvu za walimu wenyewe na hakuna mfadhili wa nje wala wa ndani anayewasaidia katika utekelezaji wa mradi huo maalum wa kujenga ofisi katika kila mkoa, ambapo katika ofisi hizo kutakuwa na eneo kwa ajili ya Benki ya walimu ambayo itakuwa inatoa fursa ya mikopo kwa wanachama walimu kwa riba ndogo katika kumuwezesha Mwalimu kumudu hali ya maisha na kujitegemeza kiuchumi.

    Katibu huyo wa chama cha walimu mkoa wa Pwani (CWT), MWL. NEHEMIAH JOSEPH ametoa wito kwa kwa walimu kujenga umoja na mshikamano miongoni mwao ili kujenga msingi imara ambao hautatetereshwa na kitu chochote kwa kuunganisha nguvu zao katika kujiimarisha kiuchumi.
    END.

No comments:

Post a Comment