Thursday, May 17, 2012

MANCINI AANZA KUJIZATITI

MANCHESTER, England
KOCHA wa Manchester City, Roberto Mancini amesema anatarajia uongozi wa klabu yake utamruhusu kutumia fedha nyingi kwa ajili ya usajili wa msimu ujao wa Ligi Kuu na mashindano ya kimataifa.

Mancini hivi sasa mpango wake ni kuhakikisha anakuwa na kikosi bora ili achukue ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya England.

Mpaka sasa Man City imeshatumia fedha nyingi kwa wachezaji walioiwezesha timu hiyo kutwaa ubingwa wa England tangu timu hiyo ilipochukuliwa na tajiri wa Abu Dhabi, Sheikh Mansour mwaka 2008.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa klabu hiyo, Khaldoon al-Mubarak yeye alisema hakuna haja ya kutumia fedha nyingi hivi sasa kwa ajili ya usajili kwa sababu Man City ina kikosi imara, lakini kocha Mancini yeye anataka kununua wachezaji wengine wenye majina makubwa.

Mancini alisema,"Barcelona na Real Madrid kila mwaka zinanunua wachezaji wawili au watatu na zinatumia fedha nyingi, nafikiri Manchester City na yenyewe itakuwa hivyo."

Alisema,"inabidi kuboresha kikosi, tunahitaji nguvu zaidi kucheza Ligi ya Mabingwa na Ligi Kuu ya England."

Katika misimu miwili iliyopita klabu za Real Madrid na Barcelona zilitumia kiasi cha pauni 105 milioni kwa ajili ya usajili.

Barcelona ilimnunua David Villa kwa pauni 34.2 milioni mwaka 2010 na miezi 12 baadaye walitumia kiasi kama hicho kumnunua Cesc Fabregas.

Madrid wenyewe tangu mwaka 2009 walimsajili Cristiano Ronaldo kwa pauni 80 milioni pia Kaka na Karim Benzema walisajiliwa kwa kiasi cha pauni 170 milioni kwa pamoja.

Mwaka jana Man City ilitumia kiasi cha pauni 197 milioni kufanya usajili, lakini mwaka huu inataka kutumia pia fedha nyingi kwa sababu inataka kumsajili mshambuliaji wa Arsenal, Robin Van Persie na kiungo wa Lille, Eden Hazard.

"Tunatakiwa kuwa na kikosi imara kwa sababu mwaka wa kwanza tulichukua kombe la FA, mwaka wa pili tumechukua ubingwa wa Ligi Kuu, mwaka wa tatu tunatakiwa kuchukua ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya,"alisema Mancini.

Mancini hivi karibuni pia anatarajiwa kuanza mazungumzo mapya na uongozi wa Manchester City kwa ajili ya kuongeza mkataba wa kuendelea kuinoa timu hiyo.

No comments:

Post a Comment