Saturday, December 31, 2011

MABOMU YAHAMIA MISIKITINI NCHINI NIGERIA

Boko Haram waendeleza mashambulizi
Boko Haram wameelekeza mashambulizi misikitini
Mlipuko mkubwa umetokea karibu na msikiti katika mji wa Maiduguri, kaskazini mwa Nigeria, ambapo watu kadhaa wameripotiwa kuuwawa.
Walioshuhudia wanasema wameona miili ya watu wanne waliouwawa.
Msemaji wa jeshi la Nigeria akizungumza na BBC amelaumu kundi la Kiislamu la Boko Haram kwa shambulizi hilo.
Kundi hilo ambalo limekuwa likitaka kulazimisha kuwepo utawala wa sharia nchini Nigeria, limeendesha mashambulizi kadhaa, zaidi kaskazini mashariki mwa nchi.
Limekiri kufanya mashambulizi kadhaa siku ya krisimasi yaliyolenga makanisa, na yaliyouwa watu wasiopungua 42.
Kundi la Boko Haram katika siku zilizopita pia limeshafanya mashambulizi dhidi ya mashirika ya kimataifa, na pia dhidi ya viongozi wa Kiislamu wa madhehebu yanayolipinga.
Msemaji wa Jeshi alisema lilikuwa shambulizi baya lakini hakueleza idadi ya watu walioathirika.
Maelfu ya watu wametoroka makwao mjini Maiduguri na miji mingine iliyoshambuliwa na Boko Haram.
Siku ya Alhamisi Rais wa Nigeria Goodluck Jonathan aliwaita wakuu wa jeshi kwenye mkutano kujadili namna ya kukabiliana na tishio la Boko Haram.
Viongozi wa Chad na Cameroon, ambazo ziko karibu na Maiduguri wameripotiwa kufanya mazungumzo kuhusu namna wanavyoweza kusaidia kuzuia kuenea kwa ghasia zinazosababishwa na kundi hilo ndani ya mipaka yao.
Kundi hilo, ambalo shina lake ni mjini Maiduguri, mwaka huu lilifanya mashambulizi ya kujitoa muhanga kwenye makao makuu ya umoja wa mataifa na makao makuu ya Jeshi la Polisi katika mji mkuu Abuja.
Pia lilihusika na mashambulizi kadhaa ya mabomu katika mji wa Jos , kati kati mwa Nigeria, katika mkesha wa Krisimasi mwaka 2012, na vile vile mashambulizi kwenye kituo cha kijeshi mjini Abuja katika mkesha wa mwaka mpya 2011.

No comments:

Post a Comment